Pages

Wednesday, 3 June 2015

Machuppa awapa Simba akili mpya

MSHAMBULIAJI nyota wa zamani wa Simba na Taifa Stars, Athuman Machuppa, ameiangalia Ligi Kuu Bara msimu wa 2014-2015 uliomalizika mwishoni mwa wiki na kutoa yake ya moyoni.
“Ligi ilikuwa tamu, nilikuwa naifuatilia, lakini imejaa kasoro nyingi kuanzia uamuzi wa marefa, viwanja, wadhamini na timu kutojipanga, ni lazima TFF iongeze kusaka wadhamini na hata klabu ziwe na wadhamini wengi ili kuwe na ushindani zaidi na ligi bora,” alisema.
“Viwanja ni tatizo, hatuwezi kuona ubora wa wachezaji wenye vipaji kama viwanja ni bomu ni Tanzania pekee zaidi ya mechi tano zinalazwa viporo na kuchezwa kwa siku mbili, hili ni lazima TFF ilibadilishe soka ni viwanja vipaji vinaonekana kwenye uwanja nzuri.
“Hata sisi mafanikio ya mwaka 2003 yalianzia kukusanywa tangu mwaka 1999 kwa vile tulipokewa vema na wazoefu tuliowakuta na kutunzwa vema kwa miaka mitatu na kuja kuwa tishio ndani na nje ya nchi, hata Simba ya sasa inapaswa kupewa muda ina vijana wenye vipaji.
“Kikosi kisipanguliwe, penye mapungufu paboreshwe na vijana wasiyumbishwe kwa kubadilishiwa makocha kila mara, wastani wa miaka 23 walionao wachezaji ni msaada mkubwa kwa Simba kuja kutetemesha Afrika mbele ya safari, vijana wana vipaji sana.”
Machuppa anayeishi Sweden alikokuwa akicheza soka la kulipwa, alizikumbusha pia klabu za soka nchini akisema: “Wazawa wathaminiwe kama wanavyothaminiwa wageni, itasaidia kujenga umoja ndani ya timu, ubaguzi unaofanywa kwa kuwathamini wageni na kuwapuuza wazawa wenye mchango mkubwa katika timu ni tatizo.
“Nazipongeza Yanga kwa kutwaa ubingwa na Azam kwa kushika nafasi ya pili, nazikumbusha kufanya maandalizi mapema kwani tiketi za kimataifa wanazo, hivyo wasilaze damu kisha kuja kutuaibisha mwakani, zijipange zicheze hatua ya makundi,” alisema.
Ligi ya Bara ilimalizika Jumamosi Yanga ikitangazwa mabingwa kwa kukusanya pointi 55, kisha kufuatiwa na Azam wenye pointi 49 na Simba wakishika nafasi ya tatu kwa pointi 47, huku Polisi Moro na Ruvu Shooting zikishuka daraja.

No comments:

Post a Comment