| Simon Msuva |
Mvua zimekuwa kero kubwa kama ilivyokuwa katika
siku za hivi karibuni jijini Dar es Salaam. Accra hadi usafiri umekuwa
ni tatizo kubwa ambako watu wanalazimika kutembea kwa miguu kwa vile
magari hazitembei kutokana na madaraja kuvunjika, barabara kuharibika
pamoja na foleni. Hali hiyo imemboa Pluijm lakini amemaliza likizo
yake na kesho Jumapili usiku atatua Dar es Salaam kuanza kibarua cha
kuisuka Yanga.
Jana Ijumaa alipiga stori mbili tatu na Mwanaspoti
akitaka kujua hali inavyoendelea nchini lakini akadokeza jambo moja
linalohusu usajili wa Yanga.
Kocha huyo alisema kwamba nguvu zake sasa ameelekeza kwa
wachezaji watatu tu na kati yao anataka wawili wawe kiboko ya Simon
Msuva na Juma Abdul.
“Ukiangalia Msuva (Simon) anaweza kuondoka wakati
wowote, ni lazima tujiandae kwa kupata mtu kama yeye au zaidi lakini pia
nataka beki wa kulia mwenye makali zaidi ya Juma (Abdul) kuongeza
ushindani hapo tunaweza kusema kidogo tumekamilisha timu yetu,”alisema
Pluijm.
“Najua kila kitu kinachoendelea huko, nafurahi
kuona kuna kazi nzuri imefanyika waliosajiliwa naamini watatusaidia
lakini bado tunahitaji watu hao zaidi.”
Pluijm amemtaja mshambuliaji Donald Ngoma wa Zimbabwe kama mmoja wao ingawa Wabongo hakuwataja.
Mholanzi huyo alisema mbali na Ngoma ambaye
usajili wake akitoka FC Platinum umezuiwa kwa muda wakisubiri maamuzi ya
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) juu ya idadi ya wachezaji wa kigeni,
pia anataka apatikane kiungo wa pembeni mmoja hasa kulia huku pia
akitaka beki wa kulia atakayesaidiana na Juma Abdul.
Alisema pia anataka kuja kuangalia uwezo wa kiungo
raia wa Sierra Leone Lansana Kamara ambaye amemtaka kusubiri jibu lake
kwa siku chache baada ya kuanza majaribio. Lakini habari za ndani ya
Yanga zinadai kwamba Kamara amewaambia viongozi kwamba yeye amekamilika
na si mtu wa kujaribiwa.
No comments:
Post a Comment