Pages

Monday, 14 September 2015

UNHCR yataka wakimbizi kushughulikiwa

Umoja wa mataifa umeelezea masikitiko yake dhidi ya mataifa kadhaa ya bara Ulaya, ya namna yanavyozingatia sheria mbalimbali zinazokinzana kuhusiana na mipaka yake.

Shirika linalowashughulikia wakimbizi UNHCR, linaonya kuwa hatua hii itawaacha maelfu ya wakimbizi katika hali ya kutatanika kisheria.

Shirika hilo la UNHCR, linasema kwamba muungano wa bara Ulaya, unafaa kubuni vituo vya kuwapokea wahamiaji, kuwaandikisha na kuwapiga msasa wahamiaji na wale wanaotafuta makao huko hasa wanaowasili nchini Ugiriki, Italia, na Hungary.

Kupitia taarifa kabla ya kufanyika kwa mkutano unaowaleta pamoja mawaziri wa haki na sheria wa muungano wa ulaya hatimaye leo Jumatatu, shirika hilo linasema kuwa mataifa ya bara Ulaya yanahitajika kuharakisha kubuni taratibu au sheria ya kushughulikia mpango huo wa wahamiaji.

Mataifa ya Ujerumani, Austria na Jamhuri ya Czech yametoa ulinzi mkali katika mipaka yao. Ujerumani inasema kuwa, imetamaushwa na ongezeko la wahamiaji wanaoingia nchini humo.
Takriban wahamiaji elfu 16 waliingia katika mji wa Munich pekee, mwishoni mwa juma.

No comments:

Post a Comment